WADUDU WAHARIBIFU WASHAMBULIA MAHINDI, HATUA ZA HARAKA KUCHUKULIWA

Untitled2

Afisa kilimo kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Musoma Godfrey Katima (aliyesimama) alipotembelea baadhi ya mashamba ya wakulima ili kushuhudia uharibifu wa zao la Mahindi kwa baadhi ya mashamba yaliyopo kijiji cha Murangi. Kulia ni Abel Biswalo akiwa katika hatua ya palizi.

Na Mwandishi wetu

IDARA ya kilimo kupitia Afisa Kilimo kutoka Halmashauri ya wilaya ya Musoma Godfrey Katima wamejiridhisha kuwepo kwa wadudu waharibifu wanaoshambulia zao la mahindi katika mashamba mbalimbali ya wakulima yaliyopo Musoma vijijini.

Hayo yamebainika kufuatia ziara ya afisa huyo kwenye mashamba ya mahindi na kukutana na baadhi ya wakulima kijijini Murangi katika kata ya Murangi ambapo alishuhudia kuwepo kwa tatizo hilo.

Awali akizungumza na afisa kilimo huyo, mmoja wa wakulima wa mahindi Christopher Magoti alisema, mahindi yao yameanza kupatwa na tatizo la kushambuliwa na wadudu mapema tu baada ya zao hilo kufikia katika hatua ya palizi.

Mkulima huyo alisema, wadudu hao wanashambulia zaidi majani laini yanayochipua, pamoja na kutoboa majani ya zao hilo jambo ambalo limekuwa endelevu na sasa linaonekana kuwa sugu kwani hawajapata ufumbuzi wowote wa kuweza kudhibiti tatizo hilo.

“Tukienda kwa maafisa kilimo wanatuelekeza dawa za shilingi arobaini elfu (40,000) wakati mimi hata chakula kwa siku ninashindia uji, tunaomba wakulima tusaidiwe hili, bila kusaidiwa basi hata hii mvua inayonyesha haitakuwa na faida kwetu na tutakufa na njaa kabisa” alisema na kuomba Mzee Magoti.

Mkulima mwingine Abel Biswalo alitahadharisha serikali kuwa endapo idara ya kilimo ya wilaya ya Musoma isipokuwa makini na kutimiza wajibu wake basi wilaya yao itakuwa na matukio ya njaa yasiyokoma kutokana na kupuuza majukumu yake, kwani kumekuwa na matukio ya muendelezo hasa katika sekta ya kilimo katika wilaya ya Musoma.

“Zao la muhogo lilishambuliwa, zao la viazi likavamiwa na wadudu kama ilivyo sasa kwenye mahindi na sasa mahindi nayo yamefikiwa na kama kawaida ya viongozi husika hatujajua tatizo hili litaisha lini” alibainisha Abel.

Kwa upande wake, Nyangai Ching’oro hakusita kulinganisha hali halisi iliyopo kwenye jamii zao na tatizo lililowakumba wakulima kwa sasa na kusema: “kwa kipindi kirefu jamii ya Musoma imekumbwa na tatizo la upungufu wa chakula uliosababishwa na ukame wa muda mrefu, lakini kwa sasa mvua imenyesha na wakulima wamelima kwa wingi. Tatizo kubwa lililopo ni mazao kushambuliwa na wadudu waharibifu kitu ambacho kitapelekea kuwepo na ukosefu wa chakula zaidi”

“Tumelia sana na tatizo la upungufu wa chakula kwani mvua ilikuwa hainyeshi. Mvua imenyesha, tumelima lakini mazao yanaharibiwa. Tusipokuwa makini tatizo la njaa halitokwisha na mimi naomba idara ya kilimo itimize majukumu yake kwetu wakulima ili matatizo haya yatatuliwe” alisema na kuomba Ching’oro.

Akizungumza baada ya kusikiliza vilio vya wakulima hao, Godfrey Katima aliahidi kuwasilisha taarifa ya tatizo hilo katika idara yao ya kilimo kwa ajili ya kuchukua hatua haraka iwezekanavyo ili kuokoa zao hilo huku akiwataka maafisa kilimo wa kata na vijiji kuwa karibu na wakulima kwa ajili ya msaada na ushauri zaidi.

“Poleni sana kwa tatizo hili linalowakabili. Kweli ni tatizo linalostahili hatua za haraka zaidi na mimi nitaliwasilisha kwenye idara yetu kwa ajili ya hatua zaidi. Pia niwatake maafisa kilimo wa kata na vijiji wawe karibu na wakulima na wawe tayari kutoa ushauri na msaada pale panapostahili” alisema na kuagiza Katima.

SHULE ZA MSINGI JIMBO LA MUSOMA VIJIJINI KUBORESHA MAKTABA ZAKE

Untitled

Moja ya maktaba zinazopatikana kwenye shule za msingi za jimbo la Musoma vijijini ambazo zipo kwenye mkakati wa kuboreshwa.

Na Fedson Masawa

SHULE za msingi zenye maktaba katika jimbo la Musoma vijijini zimeahidi kuboresha maktaba zao ili kuziweka katika mazingira mazuri zaidi ya kujisomea watoto pamoja na wananchi wenye uhitaji wa kujisomea kutoka nje ya shule hizo.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Burungu, Mkama Ng’aranga, alisema shule yake ina mpango wa kupanua maktaba hiyo ili kutoa fursa kwa wanafunzi wengi kuingia na kujisomea.

“Shule yangu ina mpango wa kupanua maktaba hii ili kutoa fursa kwa watoto kutoka shule nyingine na wananchi wa kawaida kuingia na kujisomea bila shida yoyote. Pia utaratibu huu utakuwa ni kivutio kwa vijana wa vijijini kuja kujisomea na niombe walimu wenzangu wakilifanya hili basi tutakuwa mfano wa kuigwa” alisema Mwalimu Ng’aranga.

Akizungumzia umuhimu wa kuwepo kwa maktaba bora, Mwalimu Paschal Aloyce ambaye ni msimamizi mkuu wa taaluma shuleni hapo, alisema maktaba hiyo itatoa hamasa kwa wanafunzi wa shule hiyo kwani mazingira bora ya wanafunzi kujisomea ni njia moja wapo ya kuwa na ufaulu bora katika shule, hivyo basi kuwa na maktaba kubwa na bora ni kuongeza ufaulu bora kwa wanafunzi wao.

“Maktaba bora shuleni ndio ufaulu bora wa wanafunzi. Kuwa na maktaba bora hapa shuleni naamini kabisa vijana watajituma na hawatotumia muda wao mwingi kuzurura mitaani. Hivyo matokeo yao yatakuwa mazuri zaidi” alieleza mwalimu Aloyce.

Aidha, Magreti Trutumbi ambaye ni mwanafunzi wa darasa la saba shuleni hapo, ametoa shukrani zake za dhati kwa viongozi wa serikali na shule kwa kuwajengea maktaba na kujaza vitabu kwani haikuwa hali ya kawaida kwa wao kupata eneo sahihi la kujisomea na sasa wamelipata.

Kwa upande wake Filimon Elifath alishukuru kwa mchango mkubwa anaotoa Mbunge wao Prof. Muhongo ikiwa ni pamoja na vitabu, madawati, mifuko ya saruji na mabati kwa ajili ya kufanikisha mazingira bora ya taaluma yao katika shule zote za jimbo lao.

“Tunamshukuru mbunge wetu Prof. Muhongo kwa mchango wa mabati, saruji na vitabu anavyotupa. Itatusaidia katika kufaulu masomo yetu. Nasisi wanafunzi tunaahidi kufanya vizuri zaidi kwenye mtihani wetu wa mwisho” alishukuru na kuahidi Filimon.

MBUNGE ATOA MBEGU ZA MIHOGO NA MTAMA KWA WAKULIMA JIMBONI

Untitled

Wananchi wa Kata ya Nyegina wakikabidhiwa mbegu za mihogo na mtama kwa ajili ya kuanzisha shughuli za uzalishaji wa mbegu hizo.

Na Mwandishi wetu.

MBUNGE wa jimbo la Musoma vijijini na Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo, ametoa mbegu za mtama na mihongo kwa wananchi wa jimbo hilo ikiwa ni hatua muhimu ya kupambana na tatizo la njaa.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo la ugawaji wa mbegu lililofanyika kwenye kijiji cha Nyegina, msaidizi wa Mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Ramadhani Juma alisema, hatua hiyo ya ununuzi wa mbegu ilichukuliwa baada ya Prof. Muhongo kupokea taarifa kutoka kwa wananchi wake waliohitaji msaada wa mbegu bora za mihogo na mtama.

“Kuna baadhi ya wananchi walimuomba mheshimiwa mbegu za mihogo na baadhi wakawa wamemuomba mbegu za mtama na mihogo. Prof. Muhongo aliagiza taarifa ya mahitaji ambapo Halmashauri wakawa wanahitaji gunia 700 ambazo ziligharimu Milioni 14. Baada ya kupokea taarifa hiyo tulienda kuwalipa Magereza Kiabakari Milioni 7 awamu ya kwanza ambayo sasa imeleta magunia 350 na ndio sasa yanasambazwa” alisema Juma.

Aidha, akizungumzia mbegu za mtama, msaidizi huyo alisema mbunge alitoa Milioni 1.2 ambazo zimetumika kununulia kilo 900 za mtama ambazo zitasambazwa  kwa wakulima.

“Kuhusu mbegu za mtama, kuanzia jana nimezigawa Majita, lakini pia tuna wasiwasi kwamba hizi mbegu za mtama, tutakapokuwa tunazigawa kuna wananchi wetu wataenda kusaga unga. Kwa hiyo tupate utaratibu, zile kaya zitakazochukua mtama ziandikwe na kwa kushirikiana hata na uongozi wa kijiji, wawe wanaenda kuwatembelea ili kujiridhisha kama kweli walipanda. Kwa hiyo niwaombe tuzitumie kama mbegu ili baadaye tupate mbegu nyingi zaidi” alisema Ramadhani Juma.

Kwa upande wake diwani wa kata ya Nyegina Majira Mchele amewataka vijana wajitokeze kushiriki kikamilifu katika kufanya shughuli za kilimo mashambani kwa ajili ya kuzalisha kwa matumizi ya baadaye siyo kuwaachia wanawake huku wao wakizurura mitaani.

“Mimi naomba vijana twendeni mashambani. Ukienda saa 12 saa 3 umetoka utaendelea na majukumu yako ili tumvushe yule mama anayeenda shambani mwenyewe. Hii mvua ni ya kukimbizana nayo, tujitume” alisisitiza diwani Mchele.

Naye Kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Musoma, Paul Makuli ambaye pia ni Afisa Kilimo wa wilaya alieleza utaratibu wa mgawanyo wa mbegu hizo kuwa zitapandwa katika ekari 87.5 kwa halmashauri nzima ambapo vikundi 9, taasisi 17 na kaya 100 zitapewa mbegu.

Akizungumza na wananchi wa Nyegina katika uzinduzi huo, Vicky Mbunde ambaye ni Kaimu mkuu wa Wilaya alimpongeza Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini kwa juhudi kubwa anazozifanya ndani ya jimbo hilo huku akikemea tabia ya wafugaji wanaoingiza mifugo kwenye mashamba yaliyolimwa.

“Wale ambao mnafuga mifugo hakikisheni mifugo yenu mnaitengea maeneo ambayo hayajalimwa ili angalau tunayoyafanya hapa yaonekane yana faida, atakayekiuka utaratibu huu, basi sheria ichukue mkondo wake dhidi yao” alisema.

Pia Kaimu mkuu wa wilaya ametoa onyo kali kwa vijana wanaojihusisha na matendo ya ulevi huku wakishindwa kushiriki kikamilifu katika uzalishaji na kuwataka kila mmoja ashiriki kikamilifu katika uzalishaji.

“Najua mtu hawezi kwenda kulima akiwa ametumia dawa za kulevya au ametumia kilevi chochote, najua sasa hivi serikali inapambana vikali katika kudhibiti dawa za kulevya. Sasa wenye vilabu, vilabu vyote fungua kuanzia saa 9:30 jioni. Ukifungua kuanzia saa 4 au saa 5 asubuhi, mtendaji wa kata inabidi uwakamate na uwapeleke kwenye baraza la kata mara moja” alisema Vicky.

Akihitimisha zoezi la ugawaji wa mbegu hizo, Kaimu mkuu huyo wa wilaya amewasihi wananchi kushiriki kikamilifu kila mmoja na kila kaya kuwa na shamba lililolimwa na kupandwa.

“Ukaguzi utakuja kufanyika, kila kaya moja lazima iwe na zao la chakula, aidha ulime mtama ekari moja, ulime mahindi, viazi au mihogo. Tutafanya ukaguzi wa nyumba kwa nyumba, tutakuwa na mwenyekiti wa kijiji, mwenyekiti wa kitongoji ili kubaini kila kaya na shamba lake na tujitahidi sana kulima mazao yanayostahimili ukame na madiwani na viongozi wengine mtusaidie kuhamasisha” alisema Vicky Mbunde.

 

MKUU WA WILAYA AFUNGA RASMI MAFUNZO YA UTENGENEZAJI VIFAA VYA UMEME JUA

Untitled

Vijana waliohitimu mafunzo ya kutengeneza chaja za simu na taa kwa kutumia mionzi ya jua wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa kufunga mafunzo hayo katika kituo cha Nyegina. Waliosimama nyuma ni Dkt. Hong-kyu Choi (aliyevaa fulana nyekundu), anayefuatia kuelekea kulia ni Mkuu wa wilaya ya Musoma Dkt. Vincent Naano Anney. Kushoto kutoka kwa Dkt. Choi ni Majira Mchele diwani wa kata ya Nyegina.

 

Na Fedson Masawa

MAFUNZO ya kutengeneza chaja za simu na taa zinazotumia mionzi ya jua yamefungwa rasmi huku vijana 97 wakihitimu mafunzo hayo ya siku 20.

Mafunzo hayo yamefungwa na Mkuu wa wilaya ya Musoma vijijini Dkt.Vincent Naano Anney katika kata ya Nyegina, ambapo yalitarajiwa kushirikisha vijana 100 kutoka jimbo la Musoma vijijini, lakini ni vijana 97 pekee wamehitimu baada ya vijana watatu kushindwa kushiriki kwa kutoa hudhuru.

Mbali na vijana hao,  viongozi mbalimbali wakiwemo Mwenyekiti wa kijiji cha Nyegina, Diwani wa kata ya Nyegina nao walipata fursa ya kuhudhuria mafunzo hayo yaliyoendeshwa na Dkt. Hong-kyu Choi kutoka Korea.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Nyafuru Magere kutoka kijiji cha Nyasulura alisema, ingependeza zaidi kama watajengewa kiwanda ili ujuzi walioupata kwa ajili ya uzalishaji na kujiajiri wenyewe.

“Mimi nampongeza Waziri na mbunge wetu Prof. Muhongo kwa kutuletea mafunzo haya, tumepata ujuzi wa kutosha na sasa tulikuwa tunaomba watujengee kiwanda ili tujiajiri. Vilevile napenda kuwasihi vijana wenzangu ambao hawajashiriki mafunzo haya, wasitegemee ajira kutoka serikalini, ajira ni wao wenyewe na ujasiliamali tunaoufanya ni ajira tosha” alisema Nyafuru na kuwasihi vijana wenzake wasipuuze fursa za kujiajiri.

Naye diwani wa kata ya Nyegina, Majira Mchele alimshukuru Dkt. Hong-kyu choi kwa kutumia muda wake mwingi kuwafundisha vijana wa Tanzania na Musoma vijijini na kumpongeza mbunge wa jimbo hilo kwa kuwa na uhusiano mzuri na Dkt. Choi na ubalozi wa Korea kwani ndiye aliyefanya vijana hao kuelekea kutimiza ndoto zao.

“Namshukuru sana Dokta Choi kwa kutumia muda wake, yeye ni mtu wa Korea, lakini ameamua kuugawa muda wake kwa ajili ya kuja kuwasaidia watanzania. Nimshukuru pia mheshimiwa mbunge kwa kufanya urafiki na Dokta mpaka akaibua hiki tunachokuja kukivuna. Bila Prof. Muhongo Dokta asingeijua Tanzania, wala Musoma vijijini na wala elimu hiyo msinge ipata” alisema diwani Majura.

Kwa upande wake Dkt. Hong-kyu alisema, vifaa anavyofundisha na kuvitengeneza ni muhimu na ni rahisi mno, hivyo vitawasaidia vijana kutengeneza ajira, kutoa elimu na kuboresha maisha ya watu na hatimaye vijana kufikia ndoto na matarajio yao ya usoni.

Aidha, Dkt. Choi alimshukuru Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo kwani alipokutana naye kwa mara ya kwanza ofisini kwake akiwa na vifaa hivyo, mbunge huyo alivutiwa navyo na kumuomba  akawafundishe vijana wake 100 jimboni.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo, Mkuu wa Wilaya ya Musoma Dkt. Vincent Naano Anney, aliwashukuru  wasaidizi wa Mbunge kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa kuwaunganisha wananchi ndani ya jimbo hilo na hivyo kuharakisha maendeleo.

“Kwanza nawashukuru sana wasaidizi wa mbunge kwa kuweza kuwaunganisha wananchi wa Musoma. Hii ni kwa sababu nimejifunza kitu kutoka kwa Prof. Muhongo kwa kuweka watu wake katika maeneo yote ndani ya jimbo, nikimaanisha Nyegina, Mugango, Murangi, Saragana na Busekera. Hii inaleta mpangilio mzuri sana. Nawashukuruni sana” alisema Dkt. Naano.

Aidha, akizungumzia mafunzo hayo, Mkuu huyo wa wilaya, aliwataka vijana hao kutumia ujuzi walioupata kujitanua kifkra na kujiona kuwa wana uwezo wa kufanya mambo makubwa zaidi iwapo watakabidhiwa vifaa vya kufanyia kazi na kusambaza elimu kwa vijana wenzao.

Dkt. Naano pia alipendekeza uundwaji wa vikundi vinavyotambulika kwa ajili ya kujiweka katika hatua nzuri ya kupata misaada kutoka serikalini ikiwemo Halmashauri ya Musoma.

“Maarifa na ujuzi mlioupata wa kutengeneza hizi sola ndogo, sasa mna uwezo wa kutengeneza sola kubwa endapo mkipata vifaa. Pia nawaomba mjitahidi haya maarifa muwafundishe na wengine na mkitoka hapa mkaunde vikundi na vikundi hivi tutavifadhili kwa fedha za mfuko wetu wa halmashauri”

Mkuu wa wilaya Dkt. Vincent Naano Anney  alimalizia kwa kumshukuru Dkt. Choi pamoja na ubalozi wa Korea kwa kufanikisha kazi nzuri aliyoifanya katika jimbo la Musoma vijijini na kuahidi kuwaweka vijana katika makundi na kumthibitishia mkufunzi huyo kuwa, serikali inajipanga kupitia ubalozi wa Korea nchini ili kuhakikisha vifaa vinapatikana kwa urahisi kwa ajili ya kuwaendeleza vijana nchini.

 

VIJANA 20 WAHITIMU MAFUNZO KITUO CHA BUKIMA, WAAHIDI KUWA WALIMU WAZURI

Untitled

Vijana walioshiriki mafunzo ya kutengeneza taa na chaja za simu zinazotumia mionzi ya jua.

Na Ramadhani Juma

VIJANA 20 kutoka kata 6 za jimbo la Musoma vijijini walioshiriki mafunzo ya kutengeneza taa na chaja za simu zinazotumia mionzi ya jua, wamehitimu mafunzo yao katika kituo cha Bukima.

Mafunzo hayo yaliyowashirikisha vijana kutoka kata ya Rusoli, Bukima, Makojo, Bulinga, Bwasi na Bukumi yamehitimishwa rasmi 4, Machi mwaka huu katika ukumbi wa ofisi ya kata Bukima.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, vijana hao wameshukuru kupewa fursa hiyo muhimu ya kushiriki mafunzo hayo na kuahidi kuwa hawatowaangusha viongozi waliowateua na wananchi waliofanikisha uteuzi wao kwa kuhakikisha kilichofundishwa kitawasaidia kuwa walimu wa vijana wengine.

“Tunatoa shukrani zetu za dhati kwa viongozi na wananchi waliofanikisha kutupata, elimu na ujuzi tulioupata hapa ni njia bora ya kuwafundisha hata vijana wengine zaidi” alishukuru Anthony Zephania, mmoja wa vijana hao.

Kwa upande wake Ester Aloys alisema, Dkt. Choi amefungua njia nzuri kwao vijana kujiajiri bila kutegemea ajira kutoka serikalini kama ambavyo imezoeleka kwa vijana wengi.

“Dokta Choi umetuonesha njia nzuri, tumejifunza mengi ambayo mwanzo hatukuyajua na ametupatia ujuzi wa kudumu na sasa tunaweza kujiajiri na siyo kutegemea kuajiriwa tena. Vilevile endapo tutapata uwezesho kidogo wa vifaa, tutakuwa tumeisaidia sana jamii yetu ya kipato cha chini” alisema Ester.

Akizungumza wakati wa kuagana na wanafunzi wake Dkt. Hong-kyu Choi amewaambia kuwa, hana shaka na wao anaamini ipo siku watakutana tena Musoma vijijini na kuwasimika rasmi vijana wake na kuanza shughuli za uzalishaji zaidi kwani tayari wamejifunza na kuelewa nini kinatakiwa kifanyike.

Hata hivyo, Dkt. Choi aliongezea kuwa, haoni ugumu wa yeye kuagiza vifaa vya kutengenezea kutoka Korea kuja Tanzania endapo vijana hao wakiwa tayari na serikali ikawaunga mkono.

JIMBO LA MUSOMA VIJIJINI – KILIMO CHA MTAMA NA MUHOGO

Mvua zinanyesha na wanavijiji wameomba mbegu za mazao ya chakula. Mbunge amekubali kuchangia upatikanaji wa mbegu hizo: (1) Mbegu za Mihogo za Sh Milioni 7 (saba) kutoka Magereza Kiabakari (Awamu I) na (2) Magunia 10 ya mtama (mbegu) ya Sh Milioni 1.2. Halmashauri itachangia usafiri na mengineyo.
Ofisi ya Mbunge

VIJANA WA MUSOMA VIJIJINI WAAHIDI KUJIAJIRI BAADA YA MAFUNZO

Vijana wa jimbo la Musoma vijijini wakiendelea na mafunzo ya kutengeneza taa na chaja za simu zinazotumia mionzi ya jua, pichani wanaonekana wakiwa katika hatua ya uunganishaji wa mfumo wa betri, taa na seli za sola katika kituo cha Murangi.

Vijana wa jimbo la Musoma vijijini wakiendelea na mafunzo ya kutengeneza taa na chaja za simu zinazotumia mionzi ya jua, pichani wanaonekana wakiwa katika hatua ya uunganishaji wa mfumo wa betri, taa na seli za sola katika kituo cha Murangi.

Na Fedson Masawa

VIJANA wanaopata mafunzo ya utengenezaji wa taa na chaja za simu zinazotumia mionzi ya jua katika kituo cha Murangi, wameahidi kujiajiri baada ya kumaliza mafunzo yao.

Wakingumza na mwandishi wa habari hizi, vijana hao wamempongeza mkufunzi wa mafunzo hayo Dkt. Hong-kyu Choi kutokana na jinsi anavyowafundisha na kuelewa.

Awali, akizungumza na wasimamizi wa mafunzo hayo, Ester Charles kijana kutoka kijiji cha Ryasembe kata ya Murangi, alisema anatarajia kutoka na ujuzi ambao utamsaidia kujiajiri na si kutegemea kuajiriwa tena.

“Ninafurahi sana kushiriki mafunzo haya, na kwa namna tunavyoendelea naamini binafsi ninatarajia kutoka hapa na ujuzi utakaoniwezesha kutengeneza ajira binafsi, siyo kutegemea kuajiriwa na mtu” alisema Ester.

Naye, Mugenyanda Mbasa kijana kutoka kata ya Rusoli, alimshukuru Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo kwa kuwaona vijana wake jimboni na kuwatengenezea fursa zinazowapelekea kujiajiri na hivyo ujuzi watakaoupata katika mafunzo hayo utakuwa ni taa bora itakayowasaidia kumulika maisha yao yajayo.

“Binafsi nimshukuru sana mbunge wetu wa jimbo la Musoma vijijini kwa namna alivyotupa fursa tunayoweza kutumia na kuleta mabadiliko jimboni. Pia mafunzo aliyoyaanzisha ni taa itakayotusaidia kumulika maisha yetu ya usoni” alishukuru Mbasa.

Kijana mwingine Elisha Morice, kwa upande wake aliwahimiza vijana wenzake wanaoendelea na mafunzo, waliokwisha kamilisha na wale ambao hawajaanza mafunzo kuwa mwisho wa mafunzo hayo uwe ni mwanzo wa kueneza na kusambaza ujuzi huo kwa vijana wenzao ambao hawakupata fursa ya kushiriki mafunzo hayo ili kupunguza utegemezi na uzururaji kwa vijana wa Musoma vijijini.

“Ndugu zangu, mimi napenda pia kuwahimiza vijana wote tunaoendelea na mafunzo, waliokwisha hitimu na wale ambao hawajaanza kwamba, mwisho wa mafunzo haya uwe ni mwanzo wa mafunzo kwa vijana wenzetu ambao hawakubahatika kushiriki mafunzo haya ili kuondokana na utegemezi na uzururaji” alisema kijana Elisha, anayetoka kijiji cha Chumwi.

Naye, Mkufunzi wa mafunzo hayo Dkt. Hong-kyu Choi kutoka Korea, amewasihi vijana kuwa wepesi wa kubadili mtazamo wao, fikra na kujiamini kwa kujali kile anachowafundisha kwani Prof. Muhongo ambaye ni mtu pekee aliyewafanya wafike jimboni hapo na Tanzania kwa ujumla ana nia njema na jamii yake na anaweza kuwasaidia na kuwainua vijana endapo wakiwa tayari kubadilika ili kuondokana na umaskini kwa kujitengenezea ajira binafsi.

MBUNGE WA MUSOMA VIJIJINI AKAGUA MAENDELEO YA UJENZI WA MADARASA

 

Mbunge wa Musoma vijijini na Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo (mwenye fulana nyeusi) akishirikiana na wananchi wa kijiji cha Kome kwenye ujenzi unaoendelea wa vyumba 10 vya Madarasa. Mbali na kushiriki ujenzi huo, Prof. Muhongo alitoa msaada wa mifuko na bati kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa vyumba hivyo.

Mbunge wa Musoma vijijini na Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo (mwenye fulana nyeusi) akishirikiana na wananchi wa kijiji cha Kome kwenye ujenzi unaoendelea wa vyumba 10 vya Madarasa. Mbali na kushiriki ujenzi huo, Prof. Muhongo alitoa msaada wa mifuko na bati kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa vyumba hivyo.

Na Fedson Masawa

MBUNGE wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Muhongo amekagua maendeleo ya ujenzi katika shule ya msingi Kome “B” iliyopo kijiji cha Kome kata ya Bwasi.

Akizungumza shuleni hapo, Prof. Muhongo alisema ameridhishwa na hatua nzuri iliyofikiwa na wananchi wa kijiji cha Kome, kwa kuweza kujenga jumla ya vyumba sita vya madarasa hadi usawa wa lenta huku malengo yakiwa ni kujenga vyumba 10.

“Tukitaka kufanikiwa lazima twende kwa mpango. Hatuwezi kuwa na maendeleo wakati tunakuwa na mipango ya kwenda na kurudi, kwenda na kurudi nyuma” alisisitiza Prof. Muhongo.

Aidha Prof. Muhongo amewathibitishia wananchi kuwa, mifuko mingine ya saruji itawasili Musoma baada ya wiki mbili na kuwasisitiza viongozi na wananchi kujituma kuhakikisha saruji hiyo ikifika inatumika haraka iwezekanavyo, tofauti na hivyo mifuko itahamishwa na kupelekwa kwingine.

“Baada ya wiki mbili nitatoa mifuko mingine ya saruji na mkipewa saruji au mabati, msipovifanyia kazi vitahamishwa” alisisitiza Prof. Muhongo.

Akizungumzia suala la umeme na kilimo cha umwagiliaji kama lilivyo wasilishwa na wananchi wa kijiji cha Kome, Prof. Muhongo amewaondoa wasiwasi na kusema watapata umeme wa kutosha kwa kuwa bado hatua ya kusambaza umeme vijijini inaendelea.

“Ndugu zangu kuhusu umeme msiwe na wasiwasi, umeme unakuja wa kutosha na suala la umeme tunaenda awamu kwa awamu, ndani ya miaka mitano vijiji vyote vya Tanzania vitakuwa vimenufaika na umeme” alisema Prof. Muhongo.

Kuhusu suala la kilimo, Prof. Muhongo amekiri kuwepo na ukame jimboni na maeneo mengine na kuona umuhimu wa kutumia kilimo cha umwagiliaji kwa jamii zote zinazoishi kando kando mwa ziwa ambapo amemuagiza Mwenyekiti wa halmashauri na madiwani wote kulijadili na kuona namna ya kuzisaidia jamii hizo ili kuondokana na tatizo la njaa kuliko kutegemea msimu wa mvua pekee.

Naye mwenyekiti wa Halmashauri ya Musoma Charles Magoma, amemthibitishia Prof. Muhongo kuwa suala la ujenzi wa vyumba vya madarasa wataendelea kulisimamia na kufuatilia matumizi sahihi ya vifaa hivyo na kuhakikisha vinatumika kwa wakati.

Magoma ameahidi kuwasilisha hoja ya ununuzi wa mashine kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji kwa jamii zinazoishi kandokando mwa ziwa Viktoria ili waweze kujinusuru na tatizo la njaa.

“Ndugu mheshimiwa, mimi naamini yote uliyoyazungumza tutayafanyia kazi, vifaa vya ujenzi tutaendelea kuvifuatilia na suala la mashine tutalijadili kwenye vikao vyetu vya mipango na fedha ndani ya siku mbili zijazo” alisema Magoma.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Bwasi, Masatu Nyaonge, amemshukuru Prof. Muhongo kwa kuweza kufika kijijini hapo ili kujionea kazi nzuri inayofanywa na wananchi wake na kumhakikishia kuwa pamoja na wananchi wake kukumbwa na tatizo la njaa, lakini bado hawajakata tamaa ya kufanya maendeleo na bado wana uhitaji wa vifaa vya ujenzi kijijini hapo.

PROF. MUHONGO AZINDUA MAFUNZO YA KUTENGENEZA TAA, CHAJA KWA KUTUMIA MIONZI YA JUA

Na Ramadhan Juma

MBUNGE wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo amezindua mafunzo ya utengenezaji wa taa na chaja za simu zinazotumia mionzi ya jua.

Mafunzo hayo yanayofanyika kwenye kijiji cha Nyegina, yanawahusisha vijana 100 kutoka vijiji mbalimbali vya jimbo hilo, yana lengo la kutengeneza ujuzi na ajira kwa vijana hao.

Akizungumza kwenye uzinduzi huo, Prof. Muhongo alisema mafunzo hayo mbali na kuzinduliwa Nyegina, yatafanyika kwenye kijiji cha Mugango, Bukima, Busekera na Saragana ambapo kila kituo kitakuwa na vijana 20 na mafunzo yatatolewa kwa siku tatu kwa kila kituo.

Prof. Muhongo alisema, baada ya mafunzo katika vituo hivyo vitano, vituo hivyo vitavunjwa na kuunda vituo viwili, kituo cha kwanza kitakuwa Nyegina na kingine kitakuwa Murangi ambapo kila kituo kitakuwa na vijana 50 kwa ajili ya kuwafanyia mazoezi ya mwisho.

Akizungumzia soko la vifaa hivyo, Prof. Muhongo alisema, baada ya vifaa hivyo kutengenezwa, vijana hao watakuwa wanaviuza kati ya 15,000 hadi 20,000 ambapo malighafi za kutengenezea vifaa hivyo watapelekewa, hivyo amewataka vijana jimboni humo kuchangamkia fursa hiyo.

Awali, Balozi wa Korea nchini Tanzania Song Geumyoung alisema, Korea itaendelea kudumisha uhusiano wao na Tanzania na sasa takribani miaka 20 toka mataifa haya yaingie katika uhusiano wao, bado wataendelea kudumisha uhusiano huo.

Aidha, Balozi Geumyoung alisema, vifaa hivyo vitasaidia kupunguza tatizo la umeme vijijini na hata mijini hususani kwa wale wasio na uwezo wa kupata umeme na kutoa ajira kwa vijana wengi.

“Miaka 20 ya uhusiano wa Korea na Tanzania, tutaendelea kudumisha uhusiano huu na tutasaidiana na Tanzania kusambaza umeme vijijini. Vilevile vifaa hivi vitawasaidia vijana hawa kujitengenezea ajira na pia vitasaidia wanafunzi kujisomea wakati wa usiku” alisema Balozi Geumyoung.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Wilaya Musoma Vincent Naano Anney, ameishukuru serikali ya Korea kwa hatua nzuri ya kuanzisha teknolojia ya utengenezaji wa taa na chaja zinazotumia mionzi ya jua kwani ni hatua pekee ya kuondoa utegemezi na umasikini kwa vijana wa Musoma na pia kuwaomba kuendelea na jitihada hizo ili kusaidia jimbo la Musoma vijijini na Tanzania kwa ujumla.

Naye mkufunzi wa mafunzo hayo, Dkt. Choi Hong Kyu, alisema hatua ya kwanza ya mafunzo hayo ni kuwajengea vijana hao uwezo wa kujiamini na kisha watafundishwa ujuzi wa utengenezaji wa vifaa hivyo.

“Tunataka kuwatengenezea vijana ajira binafsi na hatimaye kuacha utegemezi na kuondokana na shughuli nyingine zisizo halali. Hivyo nawaomba waonyeshe ushirikiano wa hali ya juu katika kupokea kile watakachofundishwa” alisema Dkt. Choi Hong Kyu.

WANANCHI KIJIJI CHA KIEMBA WAENDELEA KUJENGA MAKAZI MAPYA

 

Kiemba 1

 

Na. Juma Shabani

WANANCHI wa kijiji cha Kiemba kata ya Ifulifu, wanaendelea na ujenzi wa nyumba mpya baada ya zile za awali kubomolewa na upepo mkali uliokikumba kijiji hicho miezi michache iliyopita.

Wananchi hao walianza ujenzi huo baada ya kupokea vifaa mbalimbali kutoka kwa mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo ambaye aliahidi kutoa msaada huo alipotembelea kijijini hapo mwishoni mwaka jana.

Wakizungumza kijijini hapo, wananchi hao walimshukuru mbunge wao kwa kuwasaidia na kuwaondoa kwenye mazingira magumu waliyokuwa nayo baada ya nyumba zao kubomoka na nyingine kuezuliwa mabati na upepo mkali uliombatana na mvua kubwa.

“Nilikuwa na hali mbaya baada ya nyumba yangu kubomoka yote na kuishia chini na vyombo vyangu vya ndani kuharibika kabisa, nikakosa mahala pa kujihifadhi, nikawa naomba kwa majirani leo hapa kesho pale, lakini baada ya mbunge wetu kupata taarifa hizo kupitia kwa wasaidizi wake, aliweza kufika sehemu ya tukio na kujionea kilichotokea na kutuhaidi vifaa vya ujenzi siku hiyo hiyo nilipokea vifaa vya ujenzi ikiwa ni mabati, saruji na misumari” alisema Nyakaita Magati.

Magati aliendelea kusema: “hivi sasa nyumba imefikia kwenye hatua ya renta, naelekea kukamilisha nyumba yangu, kwa kweli tunamuomba mbunge wetu aendelee na moyo huo huo na Mungu ambariki sana pamoja na wasaidizi wake”

Naye, Tatu Richard alithibitisha kupokea vifaa vya ujenzi kutoka kwa mbunge na sasa nyumba yake imekamilika, jambo ambalo awali hakuamini kama lingewezekana.

“Jamani mimi mjane sijui ningefanyaje, niliona maisha yangu sasa yamekuwa magumu kupitiliza baada ya nyumba yangu kuezuliwa paa lote na kutupwa pembeni, sikuwa na mtu wa kunipa msaada kabisa, lakini Mungu sio Athumani, nilishangaa baada ya kuona watu wengi sana wakija kwangu na nikamuona mbunge wetu akiwa amefika kwangu kunipa pole na kunikabidhi vifaa vya ujenzi” alisema Tatu.

Mwandishi wa habari hizi alizungumza na wananchi wengine ambao aliwakuta kwenye maeneo yao wakiendelea na ujenzi wa makazi yao mapya na kurekebisha nyumba zilizopata nyufa, ambapo wamesema zoezi hilo litakamilika ndani ya mwezi mmoja na nusu.

VIJANA 100 KUPATA MAFUNZO YA KUTENGENEZA VIFAA VYA UMEME JUA

Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (wa pili kulia) akionesha vifaa vya umeme jua ambavyo Balozi wa Korea nchini anatarajiwa kupeleka mtaalamu jimboni humo ili kuwafundisha vijana namna ya utengenezwaji wake.

Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (wa pili kulia) akionesha vifaa vya umeme jua ambavyo Balozi wa Korea nchini anatarajiwa kupeleka mtaalamu jimboni humo ili kuwafundisha vijana namna ya utengenezwaji wake.

Na. Mwandishi Wetu

UBALOZI wa Korea Kusini nchini, unatarajia kutimiza ahadi yake iliyotolewa na balozi Song, Geum-Young kuwapatia mafunzo yatakayozalisha ajira vijana wa Musoma vijijini waliohitimu Kidato cha Nne.

Balozi Song, Geum-Young alitoa ahadi hiyo mwishoni mwa mwaka jana, ambapo aliahidi kumpeleka jimboni humo mtaalamu kwa ajili ya kuwafundisha vijana namna ya kutengeneza taa na chaja ndogo kwa ajili ya kuchaji simu zinazotumia mionzi ya jua.

Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini, Prof. Sospeter Muhongo kupitia taarifa yake, alisema Dk. Hong K Choi kwa kushirikiana na Ubalozi wa Korea Kusini watatoa mafunzo hayo kwa vijana 100 kutoka jimboni mwake.

Prof. Muhongo alisema, vijana watakaopata nafasi hiyo ni wale waliomaliza kidato cha nne na wanaoishi kwenye vijiji vya jimbo hilo.

“Mafunzo yaanza tarehe 20 Feb 2017, Kijijini Nyegina. Wasaidizi wa Mbunge na Madiwani watachagua vijana watakaohudhuria mafunzo hayo” alisema Prof. Muhongo na kuongeza kuwa, kifaa hicho kikitengenezwa gharama yake ni 15,000, hivyo vijana watapewa mafunzo ya namna ya kuvitengeneza na watauza ili kujipatia kipato.

SHULE YA MSINGI KURUKEREGE WAPOKEA MIFUKO 180 YA SARUJI

Untitled

Diwani wa Nyegina Majira Mchele (kushoto) akiwa na mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kurukerege Justine Masige, baada ya kupokea mifuko 180 ya saruji  kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa.

Na Juma Shabani

WANANCHI wa kijiji cha Kurukerege wamepata matumaini ya kukabiliana na tatizo la upungufu wa vyumba vya madarasa, baada ya kupokea mifuko 180 ya saruji kutoka kwa mbunge wa Jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo.

Mmoja wananchi wa kijiji hicho Justine Bugingo, akizungumza na mwandishi wa habari hizi kijijini hapo, alimshukuru mbunge huyo kwa kuona changamoto ya upungufu wa vyumba vya madarasa na kuitafutia ufumbuzi.

“Tumekuwa na changamoto ya upungufu wa vyumba vya madarasa katika shule yetu, ila sasa kwa juhudi za mbunge wetu ametufanya kuwa miongoni mwa watu ambao sasa tunaona mwanga mkubwa wa maendeleo jimboni kwetu” alisema Bugingo.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kurukerege Justine Masige alisema: “mimi na walimu wenzangu wote tutahakikisha tunasimamia suala la ujenzi wa vyumba vya madarasa, watoto wetu wameteseka kwa muda mrefu sana kwa kusomea nje na kusababisha kiwango cha elimu kushuka kutokana na mazingira na hali ya hewa mfano jua, mvua na upepo”

Kwa upande wake diwani wa kata ya Nyegina, Majira Mchele alithibitisha kupokea mifuko 180 ya saruji ndani ya kata yake na kumshukuru Prof. Muhongo kwa hatua hiyo inayoonyesha wazi nia yake ya kutatua tatizo la upungufu wa vyumba vya madarasa kwa shule za msingi na sekondari ndani ya jimbo hilo.

“Shukrani nyingi sana zimfikie mheshimiwa mbunge, hii ni heshima kubwa sana anayotufanyia ndani ya kata, ninachoweza kusema ni kwamba, hakuna kitakacho haribika, nitahakikisha na nitasimamia vyema kabisa ujenzi wa vyumba vya madarasa yaliyo bora kabisa” alisema diwani huyo na kuongeza kuwa, atahakikisha saruji hiyo inafanya kazi iliyokusudiwa haraka.

MIFUKO 2,560 YA SARUJI YAWASILI MUSOMA VIJIJINI, YAANZA KUSAMBAZWA

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Chumwi Lucia Mjengwa (kushoto) akiwa na wanafunzi wake Mfungo Manyama (katikati) na Mafwiri Yohana muda mfupi baada ya kupokea saruji kwa ajili ya ujenzi wa madarasa shuleni kwao.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Chumwi Lucia Mjengwa (kushoto) akiwa na wanafunzi wake Mfungo Manyama (katikati) na Mafwiri Yohana muda mfupi baada ya kupokea saruji kwa ajili ya ujenzi wa madarasa shuleni kwao.

Na Fedson Masawa

MIFUKO 2,560 ya saruji iliyotolewa na Mbunge wa jimbo la Musoma vijijini na Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo imewasili jimboni humo na kupokelewa na wasaidizi wa mbunge.

Saruji hiyo ilianza kuwasili kuanzia 13, January, 2017  imeanza kusambazwa kwenye shule mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa shule mbalimbali za msingi na sekondari Musoma vijijini ikiwa ni mkakati maalumu wa mbunge wa kukabiliana na changamoto ya upungufu wa vyumba vya madarasa jimboni mwake.

Wakati huo huo Verediana Mgoma anaripoti kuwa, shule ya msingi Chumwi imepokea mifuko ya saruji 120 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa vya shule hiyo yenye upungufu wa vyumba 13.

Mwalimu mkuu wa shule ya Chumwi, Lucia Mjengwa mara baada ya kupokea mifuko hiyo, alimshukuru mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo kwa kutatua changamoto mbalimbali katika sekta ya elimu.

“Tunamshukuru sana mbunge, mpaka sasa tatizo la madawati limekwisha, lakini tuna changamoto kubwa ya upungufu wa vyumba vya madarasa, mpaka sasa shule imegawanywa kutokana na wingi wa wanafunzi, hivyo mahitaji ya vyumba ni 23 vilivyopo ni 10 na upungufu ni 13, kwahiyo tutaitumia saruji hii vizuri na kuanza ujenzi” alisema mwalimu Lucia.

Kwa upande wake mwanafunzi Mafwiri Yohana, alimshukuru mbunge kwa msaada huo ambao utawasaidia kutatua changamoto za vyumba vya madarasa.

“Sasahivi kutokana na uhaba wa madarasa, wakati mwingine tunalazimika kusomea nje na muda mwingine hali ya hewa inapobadilika, inatulazimu kubadilishana muda wa masomo, hivyo endapo changamoto ya vyumba ikipungua tutakuwa huru darasani na kusoma tufike mbali zaidi” alisema mwanafunzi huyo.

Mwenyekiti wa kijiji cha chumwi Mafwele Mkama, akizungumza na mwandishi wa habari hizi alisema, wamejipanga kukamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa ushirikiano uliopo kati uongozi na wananchi.

“Mimi kama mdhamini mkuu katika kijiji hiki, nitakuwa bega kwa bega na wananchi wangu kumuunga mkono mbunge na kuhakikisha tunafanya vizuri zaidi katika suala la taaluma” alisema mwenyekiti Mkama.

Hadi sasa, miongoni mwa shule zilizopo kata ya Nyamrandirira zilizopokea msaada wa saruji awamu ya kwanza ni pamoja na Rwanga, Nyamrandirira, Chumwi A na B ikiwa jumla ya mifuko ya saruji 240.

KIKUNDI CHA MWANGA WAVUNA MAZAO YAO, WAJIANDAA KUINGIA SOKONI

Untitled

Baadhi ya wakulima wa bustani ya Mwanga (wenye ndoo) wakionyesha mavuno yao kwa viongozi wa TANESCO na Msaidizi wa Mbunge (Mugango) walipotembelea wakulima hao wakati wakiendelea na ziara ya kuchukua takwimu za mahitaji ya umeme kwenye kata ya Nyambono.

 

 

Na. Hamisa Gamba

KIKUNDI cha vijana wanaojishughulisha na kilimo cha bustani kwenye kijiji cha Saragana, wamekamilisha msimu wa kilimo kwa kuvuna nyanya na vitunguu walivyopanda.

Kikundi hicho cha Mwanga (Mwanga Farmers), ni moja ya vikundi vilivyopata mbegu bora na mashine za kumwagilia kutoka kwa mbunge wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo.

Mwenyekiti wa kikundi hicho Amos Bwire akizungumza kwa niaba ya wenzake alisema, licha ya mafanikio ya mavuno hayo bado wana changamoto ya ukosefu wa madawa ya kukidhi mahitaji ya mazao.

“Kuna changamoto mbalimbali zinatukabili licha ya mavuno tuliyopata, kubwa ni ukosefu wa madawa kwa ajili ya kuulia wadudu, lakini pia kushuka kwa bei ya nyanya na hali ya hewa kumetuathiri kwenye msimu huu” alisema mwenyekiti Bwire.

Naye mjumbe wa kikundi hicho Magesa Mauna alisema, licha ya changamoto walizokutana nazo kwenye kilimo hicho, bado wataendelea kulima bila kuchoka ili kuunga mkono jitihada za mbunge wa jimbo hilo aliyewahamasisha kuingia kwenye kilimo cha bustani kwa njia ya umwagiliaji.

“Tunaamini mbunge ana nia njema na sisi wakulima wa bustani, hivyo tunaomba pale tutakapokuwa tumekwama katika shughuli zetu za kilimo, aendelee kutuunga mkono kama kauli mbiu yake isemavyo hakuna kushindwa, hakuna kukata tamaa kwani kilimo ni uchumi”  alisema Magesa Mauna huku akinukuu kauli ya Prof. Muhongo.

SHULE ZILIZOJENGA MAKTABA ZAPEWA ZAWADI YA KRISMASI NA MWAKA MPYA

Na. Fedson Masawa

MBUNGE wa jimbo la Musoma vijijini na waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo amegawa vitabu kwa shule sita za sekondari na shule 24 za msingi zenye maktaba ikiwa ni zawadi ya Krismasi na mwaka mpya.

Awali kabla ya kuanza zoezi hilo lililofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Etaro, Prof. Muhongo alisema hajaridhishwa na kasi ya ujenzi wa maktaba kwa shule zote za sekondari na msingi, hivyo alimtaka Mwenyekiti wa Halmashauri ya Musoma kukutana na madiwani wake ili kuhakikisha vitabu vya awamu inayofuata shule zote ziwe zina maktaba.

“Mimi kwenye suala la vitabu nitazidi kuleta, ikiwa sisi hatuna maktaba, hawa ni watoto wa watanzania wote, nitawapatia watu wengine wavipeleke maeneo mengine” alisema Prof. Muhongo.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Musoma na diwani wa kata ya Mugango, Charles Magoma, alikiri kuwepo na mapungufu katika safu ya ufuatiliaji wa ujenzi wa maktaba kwani shule nyingi jimboni hazina maktaba.

“Ni kweli ni aibu kwetu mheshimiwa, kati ya shule 20 za sekondari tunapata shule sita  zenye maktaba na kati ya shule 111 za msingi tunapata shule 24 ambazo zina maktaba. Kwa kweli ni aibu na ni kazi ngumu tuliyonayo sasa. Sasa waheshimiwa madiwani, nadhani hili tulione kuwa ni changamoto kwetu sisi ndio wahamasishaji wa shuguli za maendeleo” alisema Magoma..

Magoma aliendelea kusema: “Mheshimiwa nimeshaamua kufanya kazi, na hili tumeshaliona kwenye halmashauri yetu, tutajitahidi ili tukuunge mkono kama ulivyoamua kulihudumia jimbo lako. Mheshimiwa tukuombe radhi, tunaenda kujipanga”

MUSOMA VIJIJINI WAWEKA WAZI MATUMIZI YA FEDHA ZA MFUKO WA JIMBO

moja

Katibu wa Mfuko wa Jimbo la Musoma Vijijini na Afisa Mipango wa Wilaya ya Musoma, Mukama Rugina (aliyesimama) akizungumza wakati wa mkutano wa kujadili matumizi ya fedha za mfuko huo.

Na. Mwandishi Wetu

WAJUMBE wa Kamati ya Mfuko wa Jimbo la Musoma Vijijini wameagizwa kuhakikisha wanakagua utekelezaji wa miradi ya kilimo ya vikundi vilivyokabidhiwa vifaa kutoka kwenye mfuko huo ili kujiridhisha.

Agizo hilo limetolewa hivi karibuni na Mbunge wa Jimbo hilo, Profesa Sospeter Muhongo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati husika wakati wa mkutano wa hadhara wa kuainisha matumizi ya fedha za Mfuko wa Jimbo kwa Awamu ya Pili uliofanyika katika kijiji cha Tegeruka, Musoma Vijijini.

Ilielezwa kwamba Awamu ya kwanza ya fedha zilizotolewa kwa ajili ya Mfuko wa Jimbo hilo ni shilingi milioni 70,820,000 ambazo zilitumika kwa matumizi mbalimbali ikiwemo shilingi milioni 20,000,000 kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Murangi.

Fedha nyingine ni milioni 27,500,000 ambazo zilitumika kwa ajili ya kurekebisha nyumba na madarasa yaliyokuwa yameezuliwa na upepo kwa shule mbili za msingi, milioni 22,500,000 ilitumika kununulia mashine za umwagiliaji, mbegu za mbogamboga na matunda pamoja na dawa za kilimo na shilingi 820,000 zilitengwa kwa ajili ya kuwezesha ufuatiliaji.

Profesa Muhongo alisema ni jukumu la Kamati husika kuhakikisha fedha imetumika kwa matumizi yaliyokubaliwa na aliagiza vikundi vyenye miradi ya kilimo ambayo haijaanza vinyang’anywe vifaa vilivyokabidhiwa na vipewe vikundi vingine vyenye vyenye nia dhabiti ya kuendeleza kilomo.

“Tembeleeni hivi vikundi, mkikuta havijaanza kutumia vifaa tulivyowapatia mvinyanga’anye na vifaa hivyo vigawiwe kwenye vikundi vyenye nia ya dhati,” aliagiza Profesa Muhongo.

Akizungumzia Awamu ya Pili ya Mfuko wa Jimbo, Profesa Muhongo alisema Mfuko wa Jimbo umepokea kiasi cha shilingi milioni 38,479,000 ambazo alisema Kamati husika kwa kushirikiana na wananchi pamoja na madiwani wamependekeza zitumike kwa ajili ya kuboresha kilimo.

Alisema shilingi milioni 16,000,000 zitatumika kwa ajili ya kununulia mbegu za kisasa za mihogo za mkombozi kiasi cha vipando 532,000 ambazo zitagawiwa kwenye Kata 21 kwa ajili ya vijiji 68, na shilingi milioni 21,900,000 itatumika kununulia mashine 21 za kukamulia alizeti.

Aliongeza kuwa hapo awali alisambaza mbegu za alizeti za majaribio kiasi cha kilo 4000 ambazo alisema zimeonesha mafanikio na hivyo aliongeza mbegu zilizoboreshwa kutoka Arusha kiasi cha kilo 5000 ambazo pia zilisambazwa.

Alisema ili kujiongezea kipato kutokana na kilimo cha alizeti, wameamua badala ya kuuza mbegu, wakulima hao watauza mafuta na ndiyo sababu ya kutenga kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya mashine hizo ambazo alizielezea kuwa ni za kuzungusha kwa mikono na hazihitaji mafuta wala umeme.

“Hizi nilitoa fedha yangu na sio katika mfuko wa jimbo; na kukitokea mapungufu nifahamisheni nijazilizie,” alisema.

Akizungumzia utaratibu wa mashine hizo, alisema kila Kata itakabidhiwa mashine yake na kwamba zitafungwa kwenye ofisi za kata chini ya usimamizi wa Afisa kilimo.

MASHINDANO YA MITUMBWI MUSOMA VIJIJINI YAMALIZIKA

sita

Vijana kutoka Kata ya Suguti ambao walishika nafasi ya Tatu wakishangilia mara baada ya mtumbwi wao kuwasili kwenye eneo la kumalizia mashindano.

Na. Hamisa Gamba

MASHINDANO ya mitumbwi Musoma vijijini yaliyoshirikisha timu 12 yamemalizika kwa Kata ya Etaro kuibuka na ushindi na hivyo kujinyakulia fedha tasilimu milioni moja pamoja na kombe.

Mashindano hayo yaliandaliwa na Mbunge wa Musoma Vijijini, Profesa Sospeter Muhongo kwa ajili ya kuuaga mwaka 2016 na kuukaribisha mwaka 2017 ambapo washindi wa pili ambao ni Kata ya Nyakatende walijinyakulia shilingi 750,000 na washindi wa tatu ambao ni Kata ya Suguti kujinyakulia shilingi 500,000 na huku wanaofuatia walipata shilingi 20,000 kwa kila Kata.

Akizungumza wakati wa kukabidhi zawadi, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Musoma Vijijini na Diwani wa Kata ya Mugango, Charles Magoma, alimpongeza Profesa Muhongo kwa kuanzisha mashindano ya namna hiyo jimboni humo kwani yamekutanisha wananchi wa Musoma Vijijini kutoka pande mbalimbali za jimbo hilo.

Aliongeza kwamba mashindano hayo yameleta mwamko mkubwa miongoni mwa vijana hasa ikizingatiwa kuwa hakuna mashindano ambayo huwakutanisha vijana kwa wingi kama ilivyokuwa kwa mashindano hayo ya mtumbwi.

Kwa upande wake, mbunge wa jimbo hilo, Profesa Sospeter Muhongo alisema aliamua kuandaa mashindano hayo na mengine ya ngoma za asili na kuimba kwaya ili kuwakutanisha wanamusoma vijijini kwa maendeleo ya afya zao na jimbo kwa ujumla.

Alisema njia mojawapo ya kuwa na afya bora ni kushiriki michezo mbalimbali na hivyo aliahidi mashindano mengine ya mieleka ambayo yatafanyika kwenye Kata ya Mugango mapema mwezi Aprili.

Aliwataka wananchi hususani vijana kujitokeza kwa wingi na kwamba washindi watapewa zawadi ambayo alisema ataitangaza siku nyingine.

Aidha, alisema kila Kata iandae washiriki wawili kwa ajili ya kushiriki mieleka na wananchi wajiandae kushuhudia mashindano hayo ya kihistoria kuwahi kutokea Musoma Vijijini.

Mashindano hayo ya mitumbwi jimboni humo yalishirikisha jumla ya Kata tisa huku kila mtumbwi ukiwa na washiriki kati ya watano hadi saba na vilevile timu moja ya kimataifa ya rafiki zake na mbunge huyo kutoka Ujerumani ilishiriki na kushika nafasi ya mwisho.

‘MSIWE NA WASIWASI, HAKUNA MTU ATAKAYEKUFA KWA NJAA’

unnamed

Wananchi wa Kata ya Nyakatende wakichukua chakula kilichoandaliwa kwa ajili ya sherehe ya Krismasi.

Na. Fedson Masawa

MBUNGE wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo amewahakikishia wananchi wake kwamba, hakuna atakayekufa kwa njaa licha ya ukame wa muda mrefu unaowakabili.

Prof. Muhongo alisema hayo wakati akizungumza na wananchi wa Kata ya Nyakatende muda mfupi kabla ya chakula cha mchana cha pamoja na wananchi wa jimbo lake katika kusheherekea sikukuu ya krismasi.

Alisema, serikali imeshalitambua tatizo la njaa linalowakabili wananchi wa jimbo hilo na itawaletea chakula cha bei nafuu, hivyo hakuna hata mtu mmoja atakayekufa njaa.

“Kwa hiyo ndugu zangu, serikali inalitambua tatizo lenu, msiwe na wasiwasi, hakuna mtu atakayekufa kwa njaa, serikali itatatua tatizo hilo” alithibitisha Prof. Muhongo.

Aidha, akizungumzia kilimo cha alizeti, kilimo cha umwagiliaji pamoja na mbegu za mihogo, Prof. Muhongo amesisitiza kuwa, kwa mkulima yeyote anayehitaji mbegu za alizeti atoe taarifa ili kuongezea mbegu hizo.

Mbali na hilo, alisema fedha za mfuko wa jimbo zitaelekezwa kwenye vikundi vya umwagiliaji pamoja na kununua mbegu za mihogo ili kupambana na tatizo la njaa.

“Zile fedha za mfuko wa mbunge ambazo tumepata zaidi ya milioni 38, zote tutajadili kuziweka kwenye kilimo ili tutatue matatizo ya njaa kwenye jimbo lenu” alisema Prof. Muhongo.

MBUNGE MUSOMA VIJIJINI AKEMEA WIZI, UHARIBIFU WA MALI ZA UMMA

unnamed

Prof. Sospeter Muhongo akizungumza kwenye moja ya mikutano yake.

MBUNGE wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amesikitishwa na wizi wa dawa na uharibifu wa baadhi ya vifaa katika Kituo cha Afya cha Murangi, Musoma Vijijini na kuagiza wahusika wachukuliwe hatua.

Agizo hilo alilitoa hivi karibuni wakati akikabidhi msaada wa vifaa mbalimbali vya afya ikiwemo vitanda maalum 10, baiskeli za wagonjwa na vifaa vingine kutoka kwa wafadhili wa Australia kwa ajili ya Kituo hicho na kushuhudiwa na wananchi mbalimbali kutoka maeneo tofauti ya jimbo hilo.

Awali kabla ya makabidhiano ya vifaa hivyo, alipokea taarifa kutoka kwa wananchi kuhusiana na wizi wa dawa uliomhusisha mlinzi wa Kituo hicho pamoja na tukio la kuharibiwa kwa gari la wagonjwa alilokabidhi mwezi Machi mwaka huu.

Taarifa husika ilimkasirisha Profesa Muhongo na hivyo kuagiza wahusika wote wachukuliwe hatua za kisheria haraka iwezekanavyo ili iwe fundisho kwa wenye tabia za namna hiyo.

Akizungumzia gari hilo, Profesa Muhongo alisema lilitolewa na Serikali ya Japan kwa ajili ya wananchi wa jimbo la Musoma Vijijini lengo likiwa ni kusaidia wananchi hao kuondokana na usumbufu waliokuwa wakiupata.

Aliongeza kuwa Serikali hiyo ya Japan ilimuahidi magari mengine zaidi ikiwa gari hilo litatunzwa vizuri na kutumika kwa shughuli iliyokusudiwa.

“Hii ni aibu kubwa, hata wafadhili watatushangaa na kutucheka, dawa nyingi tulipewa na wafadhili na gari ile tulikabidhiwa ikiwa bado mpya na kwa Tanzania gari za namna hiyo zipo mbili tu, ni hapa na Muhimbili,” alisema.

Mbali na hilo aliongeza kuwa Serikali ya Japan ilitoa kiasi cha shilingi milioni 170 kwa ajili ya kuboresha Kituo hicho na kuongeza kuwa atamuomba Balozi wa Japan nchini kufanya ukaguzi wa matumizi ya fedha hiyo.

Aliwaagiza Madiwani kufuatilia kubaini hatua iliyofikiwa ya matumizi ya fedha hiyo na alisema endapo itadhihirika kuna ubadhirifu wa aina yoyote hatua za kisheria zichukuliwe ikiwa ni pamoja na kurejesha fedha hizo.

Profesa Muhongo alisema anashangazwa kupewa taarifa hiyo na wananchi huku viongozi wakiwa kimya bila kuonesha hatua walizochukua na hivyo aliwataka Madiwani kutokuwa waoga katika kuwachukulia hatua wanaofanya ubadhirifu.

Aidha, Profesa Muhongo aliwaagiza Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Dkt. Thadeus Makwanda na Kaimu Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya cha Murangi, Dkt. Josephat Karambo kuhakikisha hadi kufikia 15 Januari mwakani gari hilo liwe limetengemaa.

MUSOMA VIJIJINI WAMMWAGIA SIFA MBUNGE WAO, WAMUOMBEA AFYA NJEMA

unnamed-jpg12

Mzee wa Kijiji cha Murangi- Musoma Vijijini, Clifford Biseko (kulia) akifungua rasmi mkutano wa kujadili uchumi na maendeleo ya Jimbo la Musoma Vijijini. Wa kwanza kushoto ni Mbunge wa Jimbo hilo, Profesa Sospeter Muhongo.

Na. Mwandishi Wetu

WANANCHI wa Jimbo la Musoma Vijijini wamempongeza Mbunge wao Profesa Sospeter Muhongo kwa kufanya mambo makubwa ya kimaendeleo ndani ya mwaka mmoja.

Pongezi hizo zimetolewa na wananchi wa jimbo hilo wakati wa mkutano wa Tathmini ya Maendeleo na Uchumi ya jimbo uliofanyika hivi karibuni katika Kijiji cha Murangi, Musoma Vijijini na kushirikisha wananchi wa jimboni humo, madiwani, wadau wa maendeleo na watendaji wa Halmashauri husika.

Awali akifungua mkutano huo mzee wa Kijiji cha Murangi, Musoma Vijijini, Clifford Biseko alisema wanamusoma vijijini wanajivunia maendeleo yanayodhihirika kila kukicha kutokana na mchango wa mbunge huyo.

Aliongeza kwamba Profesa Muhongo ni mtu sahihi kwa nafasi hiyo na kuwa hawajuti kumchagua na wanamwombea afya njema ili azidi kushirikiana nao katika kusukuma gurudumu la maendeleo jimboni humo.

Alisema katika kipindi kifupi cha uongozi wake, wameshuhudia masuala makubwa ya maendeleo kwenye sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, kilimo, sanaa na michezo.

Akizungumzia suala la afya, Biseko alisema, Musoma Vijijini haikuwahi kuwa na gari hata moja la wagonjwa, lakini tangu Profesa Muhongo awe Mbunge tayari jimbo hilo linayo magari manne.

Aliongeza kuwa Musoma vijijini haikuwahi kupata ugeni wa madaktari bingwa kwa ajili ya vipimo, ushauri na matibabu lakini kwa Profesa Muhongo hilo liliwezekana kwani alikaribisha madaktari bingwa kutoka ndani na nje ya nchi ambao walitoa huduma bila malipo.

Kuhusu suala la kilimo, Biseko alisema, tangu Profesa Muhongo achaguliwe, alisambaza tani kadhaa za mbegu za zao la mihogo na alizeti ili wananchi wajikwamue kwenye umasikini.

Aliongeza kuwa, Profesa Muhongo alipeleka wataalamu mahiri wa kilimo kutoka ndani na nje ya nchi ili kufanya tathmnini ya kilimo bora ikiwa ni pamoja na kutoa ushauri wa kilimo bora.

Aidha, suala la elimu, Biseko alisema kuwa kulikuwa na uhaba wa madawati 8,000 kwa shule zote zilizomo jimboni humo na hilo lilitatuliwa bila wao kuchangishwa pia kusambaziwa shehena ya vitabu vya sayansi kwa shule zote.

Biseko alimalizia kwa kuzungumzia sekta ya michezo na sanaa alisema kuwa Mbunge ameandaa mashindano mbalimbali na vilevile kugawa vifaa vya michezo kwenye vijiji mbalimbali jimboni humo jambo ambalo alisema limehamasisha sekta husika.

PROF. MUHONGO ASHEHEREKEA KRISMASI KWA KUFANYA MAKUBWA

unnamed

Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (wa tatu kutoka kushoto waliokaa katika viti) katika picha ya pamoja na waumini wa Kanisa la Menonite mara baada ya kumalizika ibada.

Na. Mwandishi Wetu

MBUNGE wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo ametoa mifuko 300 ya saruji kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa Zahanati ya Kigeraetuma iliyopo Kijiji cha Kamuguruki, ikiwa ni zawadi ya sikukuu ya Krismasi.

Zawadi hiyo ilitolewa 25 Desemba kijijini humo katika hafla ya chakula aliyoiandaa kwa ajili ya wananchi wa Kijiji hicho pamoja na vijiji vingine.

Katika hafla hiyo Profesa Muhongo aliongozana na familia yake pamoja na rafiki zake kutoka Ujerumani ambao kwa pamoja walijumuika na wananchi wa Musoma vijijini kusherehekea.

Awali kabla ya hafla hiyo, Profesa Muhongo na ujumbe wake walishiriki ibada katika kanisa la Menonite lililopo katika kijiji cha Nyakatende na baada ya ibada hiyo walielekea katika kijiji cha Kamguruki kwa ajili ya chakula.

Mara baada ya kumalizika kwa ibada, Profesa Muhongo aliahidi kuchangia uendelezaji wa ujenzi wa kanisa hilo, na kuagiza tathmini ifanyike ya kubaini mahitaji ili achangie.

Akiwa katika kijiji cha Kamguruki, alielezwa changamoto na mahitaji mbalimbali ya kijiji hicho ikiwemo ya ukamilishwaji wa ujenzi wa zahanati husika.

“Ikiwa ni zawadi yangu ya Krismasi kwenu, nitatoa mifuko 300 ya saruji ili kuendeleza ujenzi wa zahanati,” alisema.

Profesa Muhongo alisema 26 Desemba kutakuwa na kikao cha wabunge wote wa Mkoa wa Mara kitakachofanyikia wilayani Butiama lengo likiwa ni kujadili kilimo na maendeleo ya pamoja ya Mkoa huo.

Alisema fedha za jimbo kiasi cha shilingi milioni 38 zimetumika kama ilivyokubaliwa kwa kununua mbegu za mihogo ambazo zitagawiwa kwa wananchi. “Nikimaliza huko kikao nitarudi huku kuwaletea mrejesho lakini pia kugawa mbegu za mihogo,” alisema.

Mbali na hilo, Profesa Muhongo alisema Balozi wa Korea Nchini, Song, Geum-Young anataka kutengeneza ajira kwa vijana waliohitimu Kidato cha Nne ambao hawakupata fursa ya kujiendeleza.

Alitambulisha teknolojia ya umeme jua kwa ajili ya taa na kuchaji simu ambayo alisema Balozi huyo kupitia mtaalamu wake anatarajia kuipeleka jimboni humo kwa kuwafundisha utengenezaji wake vijana hao.

“Hiki kifaa cha umeme jua kikitengenezwa gharama yake ni 15,000 kwa hiyo vijana watapewa mafunzo ya namna ya kuvitengeneza na watauza ili kujipatia kipato,” alisema.

Alisema Februari mwakani, Balozi huyo na mtaalamu wake watafika jimboni humo kwa ajili ya kutambulisha vifaa hivyo ikiwa ni pamoja na kuandaa mafunzo na hivyo aliwataka wazazi wawaruhusu vijana wao kushiriki mafunzo husika.

MAMIA WAHUDHURIA KIKAO CHA KUJADILI MAENDELEO MUSOMA VIJIJINI

musomavijijiji

Baadhi ya wananchi wa Musoma Vijijini waliohudhuria mkutano huo wakimsikiliza Mbunge wao, Profesa Sospeter Muhongo (hayupo pichani).

Na Fedson Masawa

MAMIA ya wananchi wamejitokeza kuhudhuria kikao maalumu cha kujadili uchumi na maendeleo ya jimbo lao kilichofanyika jana kwenye kijiji cha Murangi, Musoma vijijini.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na viongozi wa serikali, madiwani, viongozi wa vyama vya siasa pamoja na wasomi mbalimbali wakiwemo waliozaliwa ndani ya jimbo hilo.

Waliowakilisha serikali kwenye kikao hicho ni Mkuu wa wilaya ya Musoma Dk. Vincent Naano na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Musoma, Frola Yongolo.

Awali akizungumzia kabla ya kuanza kwa kikao hicho, Mbunge wa Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo aliwataka viongozi wa idara zote na madiwani wajipange kwa sehemu zao na kuhakikisha kila kitakachojadiliwa kinafuatiliwa ndani ya miezi minne kwa ajili ya kupima utekelezaji wa maazimio ya kikao hicho.

Mambo yaliyojadiliwa katika kikao hicho ni pamoja na Elimu, Afya na kilimo kama yalivyoainishwa kwenye vipaumbele vya jimbo la Musoma Vijijini.

Elimu

Akianza na suala la Elimu, Prof. Sospeter Muhongo amefafanua kuwa, madawati bado hayajatosha kwani ukizingatia idadi ya wanafunzi waliohitimu darasa la saba na wale walioandikishwa darasa la kwanza na upungufu wa madawati ya shule za sekondari, bado kutakuwa na upungufu wa madawati 5000 ndani ya jimbo zima.

Ili kufanikisha zoezi hili, Mbunge ameiagiza halmashauri kulisimamia na kuhakikisha hakutokuwa na upungufu wa madawati. Pia aliwaomba wote wenye moyo wa kuchangia wawasiliane na mkurugenzi wa halmashauri kupitia namba ya simu: +255754414441

“Kwa hiyo ndugu zangu hiyo kazi tunaiweka mikononi mwa halmashauri na watakaohitaji kuchangia, ni vizuri muwasiliane na mkurugenzi” alitoa utaratibu Prof. Muhongo.

Kwa upande wa ujenzi wa vyumba vya madarasa, Prof. Muhongo amebainisha kuwa, kuna upungufu wa vyumba 748 vya madarasa kwa shule zote za msingi na sekondari na tayari ameshafanya mazungumzo na JKT kwa ajili ya kupatiwa vijana watakaofanya shughuli za ujenzi wa vyumba hivyo jimboni.

Pia ameongeza kuwa vifaa ikiwemo saruji na mabati vitanunuliwa moja kwa moja kutoka viwandani na ameshakamilisha mazungumzo na makampuni mawili; TWIGA CEMENT kwa ajili ya saruji pamoja na ALUMINIUM AFRICA kwa ajili ya mabati.

Akizungumzia utaratibu wa kuchangia ujenzi wa vyumba vya madarasa, Prof. Muhongo amesisitiza kuwa, fedha zote zitakazochangwa zinakwenda moja kwa moja kwenye akaunti ya kampuni husika, jimboni vitaletwa vifaa tu na vifaa vikifika vielekezwe kwenye maeneo husika.

“Hatutoi hela mkononi, unapokea mabati na simenti, na simenti ikifika naomba iende moja kwa moja kwenye eneo husika isikae stoo” alisisitiza Prof. Muhongo.

Wakichangia kipengele cha ujenzi, wananchi na viongozi wa jimbo la Musoma vijijini wamekubaliana na Mbunge wao na kuahidi kuungana pamoja na pia kuacha malumbano ili kusukuma gurudumu la maendeleo ya jimbo hilo.

“Kinachotuumiza ni ubishi, lakini tunaamini tupo pamoja na wewe na tunaahidi kukupa ushirikiano. Pia hatutaweza kuwavumilia viongozi wazembe wa halmashauri watakaoonesha namna fulani ya kurudisha nyuma maendeleo ya Musoma vijijini” alisema Mambo Japan, Diwani wa kata ya Bulinga.

Kuhusu ujenzi wa shule za sekondari za elimu ya juu; Akigusia pia suala hilo, Prof. Muhongo amesisitiza ujenzi wa sekondari za mfano za sayansi; Mkirira, Mugango, Bugwema na Mtiro kuwa kasi iongezeke ili ifikapo mwaka 2018 ziwe tayari na ziwe zimeanza kutumika ambapo amesisitiza kuwa ni shule za masomo ya sayansi.

Kilimo

Suala la kilimo pia limezungumzwa ambapo Prof. Muhongo amesisitiza wananchi kuendelea kulima mazao ya biashara na chakula kwa ajili ya kuondokana na umaskini na kuongeza chakula kwa kila kaya.

Akizungumzia suala la mbegu za alizeti, Prof. Muhongo amesema tayari jumla ya tani 5 za mbegu za alizeti zimeshawasili jimboni na tayari wakulima wameshapewa mbegu hizo bure. Aliongeza kuwa endapo kutakuwa na wakulima wanaohitaji mbegu hizo basi watoe taarifa zinunuliwe nyingine.

“Tani 5 za mbegu za alizeti sawa na kilogramu 5000 zimeshagawiwa kwa wakulima. Kama kuna watu bado wanahitaji waseme mbegu ziagizwe tena” alisema Prof. Muhongo

Akizungumzia utaratibu wa soko la alizeti, Prof. Muhongo amewathibitishia wananchi kuwa soko la uhakika litakuwepo na pia mashine ndogo ndogo za kukamua zitatolewa kwa baadhi ya kaya ili wakamue na kuuza mafuta.

“Mwaka jana tuliuza, mwaka huu tutauza na tutakuwa na mashine ndogo ndogo za kukamua mafuta. Pia nimeshafanya mawasiliano na mmiliki wa kiwanda kikubwa cha mafuta na amenithibitishia kufika jimboni kwa ajili kununua alizeti” alithibitisha Prof. Muhongo.

Kilimo cha umwagiliaji na mbegu za mihogo; Prof. Muhongo mbele ya mamia ya waliohudhuria kikao hicho amependekeza fedha za mfuko wa jimbo Tshs. 38,479,000/= zielekezwe kwenye vikundi vya kilimo cha umwagiliaji pamoja na kununulia mbegu za mihogo na ameomba madiwani watayarishe orodha ya vikundi vitakavyonufaika na fedha hizo.

Aidha, Prof. Muhongo amependekeza pia kikao cha kuhidhinisha fedha hizo kifanyike 26, Disemba 2016 saa 9:00 alasiri kijijini Tegeruka.

Uvuvi, suala la ufugaji wa samaki; suala hili pia limesisitizwa kwa madiwani na halmashauri kutakiwa kuorodhesha maeneo ya ziwani yanayofaa kwa ajili ya ufugaji wa kisasa wa samaki. Prof. Muhongo amependekeza kikao cha ufuatiliaji wa maazimio kifanyike kijijini Bugoji baada ya miezi minne kuanzia sasa.

Afya

Wakizungumza kuhusu ujenzi wa vituo vitatu vya afya jimboni; Bukima, Nyegina na Mugango, Madiwani wa kata hizo wamesema kuwa ujenzi wa vituo umeaanza na unaendelea vizuri.

“Nyumba ya mganga boma tayari limekamilika na maboma ya wodi yapo tayari hivyo naomba halmashauri itusaidie kuezeka kwani tunatarajia kufikia 2017 tutakuwa tumekamilisha” alifafanua Mchele Majira, Diwani wa kata ya Nyegina.

Kwa upande wake Prof. Muhongo ameongezea kuwa kila mwananchi awe mlinzi wa mali zinazoingizwa jimboni ili zitumike katika matumizi sahihi na kuendelea kuwapa moyo wale wanaojitolea kulisaidia jimbo la Musoma vijijini.

Alisema kwa wale madiwani watakaopewa msaada wowote kwenye kata zao ikiwa ni pamoja na magari na vifaa vya ujenzi na kushindwa kusimamia vizuri, hatosita kupeleka kata nyingine ambako wanajali.

Halmashauri kufanyia vikao vyote Murangi

Mbunge, Madiwani, Mkurugenzi kwa pamoja wamekubaliana kwa kauli moja mbele ya wananchi wa jimbo la Musoma vijijini kuwa vikao vyote vya halmashuri vitakuwa vinafanyika Murangi. Lengo kubwa ni kutaka kuijenga makao makuu ya halmashauri ya Musoma vijijini ambayo ni Murangi.

Akizungumza na wananchi na viongozi wa ngazi zote, Prof. Mukama Biswalo mwakilishi maalum wa umoja wa Afrika huko Sudan ya Kusini ambaye pia ni mzaliwa wa Musoma vijijini alisema: “hatuwezi kuijenga halmashauri yetu wakati vikao tunafanyia mjini badala ya Murangi. Bila kufanya hivi, haiwezekani kuijenga halmashauri ya Musoma Vijijini.”

“Mkurugenzi, make history kuwa mkurugenzi wa kwanza kuanzisha makao makuu ya Musoma vijijini Murangi. Hatuwezi kuijenga halmashauri wakati hatutaki kufanyia vikao vyetu Murangi” alisisitiza Prof. Biswalo.

MBUNGE MUSOMA VIJIJINI ATOA MSAADA KWA WAATHIRIKA WA KIMBUNGA

untitled-33

Prof. Muhongo akimkabidhi vifaa Nyakaita Magati (mwenye fulana nyekundu) mifuko ya saruji 40, misumari kilo 10 na mabati 24 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba iliyoezuliwa na kubomolewa na kimbunga katika Kata ya Ifulifu.

Na Ramadhan Juma

MBUNGE wa jimbo la Musoma vijijini Prof. Sospeter Muhongo, ametoa msaada kwa kaya tano zilizoathirika na kimbunga katika kata mbili za Ifulifu na Bukima.

Msaada uliotolewa ni pamoja na mabati 105, mifuko ya saruji 105, mbao za kenchi 15 na misumari Kilo 56.

Akizungumza baada ya kukabidhi vifaa hivyo vya ujenzi, Prof. Muhongo aliwataka wananchi waliokabidhiwa vifaa hivyo wavitumie kwa matumizi yaliyokusudiwa ya kuboresha makazi yao yaliyoharibiwa na kimbunga na si vinginevyo.

Mmoja wa wananchi waliopokea msaada huo, Tatu Richard alimshukuru mbunge kwa kuguswa na tukio lililompata na kusema kuwa pamoja na kuwa na watoto wengi bado hakuona mtoto wake hata mmoja aliyeguswa na tukio hilo.

“Mimi ni mzee, ninao watoto wengi, lakini hayupo hata mtoto mmoja kati ya wanangu aliyeguswa na tukio hili. Ninamshukuru sana mbunge wangu kwa kuniona na kunisaidia” alishukuru Tatu.

Naye Nyakaita Magati alishukuru kwa msaada wa mabati 24, saruji mifuko 40 pamoja na kilo 10 za misumari na kusisitiza kuwa hakuamini kwa kile alichokifanya Mbunge huyo kuwasaidia kurudisha nyumba zao kwenye hali nzuri baada ya kuharibiwa na upepo mkubwa.

“Siamini macho yangu kama hili linalofanyika hapa kwangu ni tukio halisi. Naona kama miujiza, hakika nina kila sababu ya kukushukuru mbunge wetu kwa kutujali, kumbe kura yetu tuliiweka panapostahili na leo tunayaona matunda yake” alisema Magati kwa furaha.

Mkazi mwingine Pili Mabele aliyekabidhiwa mabati 21, mifuko 5 ya saruji na kilo sita za misumari alimshukuru Mbunge kwa msaada aliompatia na kutoa somo kwamba ni vema kumheshimu na kumthamini kila mmoja bila kujali kama ni ndugu yako.

“Hakika ni jambo la kipekee na la kushukuru hata kama ni mbunge kuja kutoa msaada kama huu kwa mtu ambaye hana imani kama alimpigia kura. Hii imetuonesha njia kuwa kila mtu lazima amjali mwenzake hata kama siyo ndugu yake” alishukuru na kueleza Pili Mabele.

Sambamba na msaada huo, Prof. Muhongo amekabidhi Jefu Kibhisa taa moja inayotumia mwanga wa jua pamoja na chaja moja ya simu inayotumia mwanga wa jua.

Akikabidhiwa vifaa hivyo ambavyo vimeenda sambamba na msaada wa mabati 23, misumari kilo 20 na saruji mifuko 50, Jefu ameshukuru na kumpongeza Prof. Muhongo kwa jitihada za kuijali jamii ya jimbo lake.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi na uongozi wa kijiji cha Kiemba, Mwenyekiti wa kijiji hicho Golo Atanas alimshukuru mbunge kwa msaada alioutoa kwa watu walioathirika na kimbunga.

Akikamilisha ziara yake katika kijiji cha Bukima kata ya Bukima, Prof. Muhongo amemkabidhi msaada wa vifaa vya ujenzi Perusi Turuka ambaye ni muhanga wa kimbunga katika kijiji cha Bukima kata ya Bukima.

Vifaa alivyokabidhiwa mkazi huyo wa Bukima ni Mifuko 5 ya saruji, mbao 15 za kenchi, mabati 10 na Kilo 10 za misumari.

Sambamba na msaada huo, Prof. Sospeter Muhongo amesisitiza suala la kilimo kuwa ndio mbinu pekee inayoweza kuondoa umaskini na njaa Tanzania hivyo wananchi wanatakiwa kulima mazao ya chakula kwa wingi na mazao ya biashara ili kuondokana na utegemezi.

“Ndugu zangu, mimi ninaamini kweli hali ya hewa haikuwa nzuri, lakini tunatakiwa tulime kilimo cha kisasa…” alisema Prof. Muhongo.

Kwa upande wake mwenyekiti wa CCM wilaya ya Musoma vijijini, Yahana Mirumbe, alimshukuru mbunge kwa jitihada za kuwa karibu na jamii nzima ya jimbo lake na kuitaka jamii hiyo kujenga nyumba bora zenye hadhi ya kuwekwa umeme ili kuepuka madhara yatokanayo na umeme ikizingatiwa wakati wowote watawekewa umeme.

KILIMO CHA MPUNGA CHAANZA TENA BAADA YA VIBOKO WAHARIBIFU KUUAWA

untitled

Bi. Nyanjagi Michael akiwa katika shughuli za kupanua shamba lake kwa ajili ya kilimo cha mpunga.

Na Fedson Masawa

MASHAMBA makubwa ya mpunga yaliyotelekezwa kutokana na wakulima kuhofia viboko waharibifu yameanza kulimwa katika maeneo tofauti ya kata za kandokando mwa ziwa Viktoria, jimbo la Musoma vijijini.

Hatua hiyo imekuja mwezi mmoja baada ya mtaalamu aliyesaidia kudhibiti tatizo la viboko waharibifu jimboni na kuwahakikishia wakulima kuanza kutumia mashamba yao bila hofu yoyote.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mkazi wa kijiji cha Bukumi, Nyanjagi Michael alisema wanashukuru mafanikio ya mtaalamu huyo ambaye amewasaidia kurudi kwenye mashamba yao na kuendelea na kilimo cha mpunga.

“Tunamuamini sana mtaalamu wetu, amefanya kazi nzuri kwa maana ameweza kuua viboko wawili hadi sasa hatuwaoni tena kama ilivyokuwa awali, mashamba yetu tuliyoyatelekeza tunahakikisha tutalima bila hofu yoyote” alisema Nyanjagi.

Katika hatua nyingine, mkazi mwingine wa Bukumi, Nyasami Mgono ameishukuru ofisi ya Mbunge kwa kazi nzuri na yenye mafanikio iliyofanyika ya kumpata mtaalamu ambaye amekuja jimboni humo kutatua tatizo lililoshindikana kwa miaka mingi.

“Binafsi naishukuru sana ofisi ya Mbunge wetu, kwa kazi nzuri inayofanyika kwani ni kazi yenye mafanikio. Tuliangaika kwa kipindi kirefu na sasa tumerudia kilimo cha mpunga kwenye mabonde yetu” alisema Mgono.

Kwa upande wake Nyangaso Mabure, alisema kwa mafanikio yaliyopatikana baada ya kudhibiti viboko waharibifu, wakazi wa maeneo ya kandokando mwa Ziwa Viktoria wataanza kunufaika na maeneo yao na kuwaomba viongozi wao kudhibiti kila dalili zozote zinazoashiria uvurugaji wa mazao yanayolimwa na wakulima katika maeneo hayo.

“Kwa hatua iliyofikiwa ya kudhibiti viboko waharibifu waliotusumbua kwa muda mrefu, tunaamini kila mmoja wetu kwenye eneo lake ataanza kulitumia bila kuhofu” alisema Nyangaso.

“Tunachozidi kuwaomba na kuwasihi viongozi wetu wanaohusika na hili tatizo wazidi kuwa na moyo kuendelea kudhibiti dalili zote zinazoweza kuharibu na kuvuruga mazao yetu” aliongeza na kuomba Nyangaso.

Afisa kilimo wa kijiji cha Bukumi, Alex Mihambo amethibitisha jitihada za wakulima wa kandokando mwa ziwa Viktoria hasa kijiji cha Bukumi kwa kurudisha imani yao na kuwasihi wakulima kwa kuzingatia ushauri wa wataalam.

“Wakulima hawa kweli wamerudisha imani yao baada ya kusumbuka kwa kipindi kirefu, sasa wameamua kulima mpunga katika maeneo haya. Ninachozidi kusisitiza ni kulima kilimo cha kisasa kwa kufuata ushauri wa kitaalamu” alisema na kusisitiza Alex Mihambo.